TAFUTA HAPA

MAMA MDOGO SEHEMU YA NNE


ILIPOISHIA,,,,,,“Mwanangu nakupenda sana wewe pamoja na mdogo wako naamini Mungu atawasaidia mimi siwezi kupona naumwa kansa ya kizazi na imefika katika hatua mbaya sana, naomba usilie ningependa kuona mkifurahi muda huu ambao tuko pamoja.” Alisema mama Jamal huku akiwa anatabasamu na kumfuta machozi mtoto wake na kumshika mkono. Mama yake  alikuwa anapata maumivu makali sana kwa wakati huo.
INAPOENDELA,,,,Kesho yake asubuhi hali ya mama Jamal ilizidi kuwa mbaya ikabidi wa mbebe kumkimbiza hospitali lakini kabla hata hawajafika hospitali mama Jamal alifariki dunia. ilikuwa ni huzuni na pigo kubwa sana katika familia yao. Mzee Said alijitahidi kuwa jasiri sana lakini kwa watoto wake ilikuwa ni vigumu walilia sana.
Siku ya mazishi ilipangwa na hatimaye mama Jamal alizikwa na umati mkubwa wa watu. Walikuwepo wafanyabiashara mbalimbali, ndugu pamoja na marafiki. Baada ya maziko watu walitawanyika na kuwaacha Jamal, Aisha pamoja na baba yao wakiwa katika wakati mgumu sana.
Kilikuwa ni kipindi kigumu sana kwa Jamal. Msiba wa mama yake ulimkuta akiwa katika maandalizi ya kufanya mitihani ya kumaliza muhula. Jamal alibaki nyumbani wakati wote na wenzake walikuja kumtembelea kumpa pole na matumaini. Ilipofika tarehe ya mitihani alikwenda kufanya mitihani na baadaye walifunga shule. Jamal alirudi nyumbani na kuungana na baba na mdogo wake. Mzee Said alijitahidi katika kila namna ili kuwaliwaza watoto wake wasiwe wapweke.
***********************Baada ya miezi saba**********************

Jamal na Aisha walianza kuzoea hali ya kuishi bila ya Mama, waliendelea kuishi vizuri. Jamal alikuwa Kidato cha Nne na Aisha alikuwa Darasa la Tano. Mzee Said aliendelea na shughuli zake kama kawaida, huku akitunza mali na kuendesha biashara alizoacha Mama Jamal.  Siku moja Baba Jamal akiwa amelala usiku aliwaza mambo mengi sana hususani kuhusu upweke baada ya kifo cha mkewe.
“Ni vigumu sana kuishi bila ya kuwa na mke, hali ya kuishi hivi mimi siiwezi kabisa itanibidi nifanye utaratibu wa kuoa mke mwingine wa kuniliwaza na kunisaidia shughuli mbalimbali hapa nyumbani, ikiwa ni pamoja na kuwatunza watoto wangu.” Aliwaza baba Jamal.
Baada ya siku kadhaa kupita alikutana na msichana mmoja aliyeitwa Sophia, msichana huyo alikuwa ni binti wa umri wa miaka Ishirini na moja. Sophia alikuwa ni binti mdogo sana kuolewa na Mzee Said, kwani angeweza kuwa hata mtoto wake wa kumzaa. Walipendana na huyo msichana na baadaye akaamua kutaka kumtambulisha kwa watoto wake ambao kwa wakati huo walikuwa wapo shule za bweni. Basi alichokifanya alimchukua yule msichana na kuanza kuishi naye pale nyumbani bila hata ya watoto wake kufahamu.
“Sophia mpenzi wangu karibu sana nyumbani, hapa ndipo ninapoishi, nina watoto wangu wawili Jamal na Aisha ambao kwa sasa wapo shule za bweni.  Ni watoto wazuri sana, najua ukiwaona utawapenda.” Alisema Mzee Said huku Sophia akiwa anamtazama.
“Asante sana mpenzi wangu. Ila …” Alishukuru Sophia lakini alipotaka kuendelea alisita kidogo.
“Ila nini?” Aliuliza Mzee Said.
“Ahmm! Ila sijui kama watoto wako watakubali mimi niwe mama yao mdogo.” Alitamka Sophia huku akimwangalia Mzee Said kwa aibu.
“Usijali kuhusu hilo mpenzi, kwani mimi nilichoamua hakuna anayeweza kunipinga. Wewe ndiye utakuwa Mama mwenye nyumba kuanzia sasa. Hapa ni kwako sawa mamaaa?” Alisema Mzee said kwa kujiamini huku akicheka.Nini kinaendelea